Thursday 26 November 2015

Acheni ujenzi holela.


HALMASHAURI ya Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa imewataka wakazi wa mji kusitisha ujenzi holela unaofanywa na wakazi hao ili kujiepusha na hasara wanazoweza kuzipata pindi watakapo bomolewa nyumba zao kutokana na kukiuka taratibu za mipango miji.

Ushauri huo umetolewa na mkurugenzi wa halmashauri hiyo Hamidu Njovu wakati akizungumza na gazeti hili lililotaka kujua mikakati  inayofanywa na halmashauri katika kukabiliana na tatizo la ujenzi holela unaofanywa na wakazi wa halmashauri hiyo kwa madai kuwa manispaa imeshindwa kuwapimia viwanja.

Alisema kuwa wakazi hao wanapaswa kufuata taratibu za mipango miji ili kuepuka kupata hasara itakapobidi kuwabomolea nyumba zao kwani baadhi yao wanajenga bila kufuata taratibu kitu ambacho ni hatari kwao na mali zao.

Mkurugenzi huyo alisema halmashauri hiyo imetenga maeneo ya viwanda na makazi ya watu lakini kitu cha kushangaza baadhi ya watu wamekuwa wakiyavamia maeneo hiyo na kujenga makazi ya kudumu kanakwamba hawajui kuwa hilo ni eneo la viwanda.

Alisema itakapofika wakati Manispaa inahitaji eneo lake kwaajili ya kuliendeleza italazimika kuwaondoa watu hao na wataanza kuilalamikia serikali wakati wao ndio walioenda kuvamia maeneo hayo huku wakijua sababu za kutengwa kwa eneo husika.

Kwaupande wake Frorian  Simbeye mkazi wa Sumbawanga mjini alisema kuwa yeye binafsi anashangazwa na agizo hilo la manispaa huku halmashauri hiyo ndiyo yenye wajibu ya kupima viwanja lakini haijafanya kazi hiyo kwa miaka mingi sasa kitu kinachosababisha wananchi wajenge kiholela.

Alisema ni lazima mkurugenzi ahakikishe anapima viwanja kila wakati na kwa wakati muafaka ili wananchi wajenge makazi yao lakini kuwalaumu kuwa wanafanya ujenzi holela wakati ofisi yake haijapima maeneo ni kutowatendea haki wananchi hao.

GURIAN  ADOLF

Polisi Katavi wanasa Jangili


JESHI la polisi mkoani Katavi limefanikiwa kumnasa jangilii anayefahamika kwa jina la Xsavery Sikazwe(43) mkazi wa kijiji cha Igongwe kata ya Sitalike Tarafa ya Nsimbo Wilaya ya Mlele Mkoani humo ambaye alikuwa akisakwa kwa muda mrefu.
Kamanda wa polisi mkoani humo Dhahiri Kadavashari alisema kuwa kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo kunatokana na ushirikiano mwema uliopo baina ya polisi na wananchi ambapo polisi walipata taarifa za siri zilizosababisha kukamatwa kwa jangili huyo.
siku ya kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo polisi waliandaa mtego nyumbani kwa mtuhumiwa huyo ambapo polisi walijificha porini karibu na nyumba ya mtuhumiwa na ilipofika majira ya saa 12;30 za jioni walimuona mtuhumiwa akirejea nyumbani kwake ndipo walipomvamia na kumtia mbaroni.
Baada ya kumkamata walianza kufanya msako katika nyumba yake na hawakufanikiwa kupata kitu ndipo baada ya kumbana mtuhumiwa huyo aliwapeleka umbali wa mita tano kutoka katika nyumba yake na kuwaonesha polisi eneo ambalo walianza kufukua na kukuta mfuko wa sandarusi ambao ndani yake kulikuwa na jino moja la tembo pamoja na mikia miwili ya mnyama huyo.
Kamanda Kidavashari alisema kuwa kutokana na kupatikana kwa mikia hiyo miwili kunaonesha kuwa mtuhumiwa huyo aliua tembo wawili ambao wanathamani ya shilingi milioni 60 ambapo anashikiliwa na polisi.
Katika tukio jingine Kamanda huyo wa polisi alisema kuwa watu watatu waliofahamika kwa majina ya Juma Kapongo(55), Amos Kapongo(20) pamoja na Haruna Sikazwe(20) mkazi wa Sitalike wilayani Mlele walikamatwa wakiwa na silaha moja aina ya gobore ikiwa na risasi yake moja.

Kidavashari alisema kuwa watu hao walikamatwa kutokana na msako unaoendelea mkoani humo wenye lengo la kukomesha ujangili unaofanyika katika ifadhi ya taifa ya Katavi na mapori yake ya akiba kwani polisi ikishirikiana na kikosi cha askari wa wanyama pori wamedhamiria kuumaliza ujangiri katika hifadhi hiyo.
Mwisho.

Acheni siasa chapeni kazi-DED

Na Gurian  Adolf





ILIYOKUWA tume ya uchaguzi jimbo la Sumbawanga mkoani Rukwa imewataka wakazi wa jimbo hilo kuachana na masuala ya siasa badala yake wajikite katika kufanya shughuli za maendeleo ambazo zitawaletea maendeleo katika maisha yao.

Mkurugenzi wa mji wa Sumbawanga Hamidu Njovu aliyasema hayo jana wakati akizungumza katika moja ya kituo cha redio kilichopo jimboni humo ambapo alikuwa akiwashukuru wananchi kwa kushiriki vizuri katika uchaguzi mkuu uliopita.

Alisema kuwa wakati wa siasa umepita na aliyeibuka na ushindi ni Aesh Hilary aliyefanikiwa kuitetea nafasi hiyo, hivyo basi hapana budi kwa wakazi wa jimbo hilo kuhakikisha wanamuunga mkono ili aweze kutekeleza majukumu yake na kuwaletea maendeleo.

Njovu alisema wakati wa kampeni watu waligawanyika katika makundi kufuatana na vyama vyao vya siasa lakini hivi sasa wakazi wa Sumbawanga mjini wanapaswa kuwa kitu kimoja na kukabiriana na maadui wakuu ambao mmoja kati yao ni umasikini.

Alisema itakuwa ni jambo la ajabu kuona baadhi ya watu wakiendelea na tofauti zao ambazo zilijitokeza katika uchaguzi mkuu kwa misingi ya itikadi za kisiasa kwani tayari wakati huo umepita na halmashauri imepata madiwani na mbunge ambao sasa wanawajibu wa kuwatumikia wananchi.

Naye Vanny Kansapa mkazi jimbo hilo alisema kuwa kinachosubiriwa hivi sasa ni kwa Hilary kuhakikisha anatekeleza ahadi alizoahidi wakati wa kampeni kwani wananchi walimpa kura wakiwa na imani naye kutokana na rekodi yake ya kuwatumikia.

Alisema kuwa moja ya changamoto zinazowakabiri wakazi wa mji huo ni tatizo la maji na kupitia mradi mkubwa unaotekelezwa na serikali ungeweza kumaliza kero hiyo lakini tatizo linaloonekana ni usimamizi mbovu ambao unasababisha mradi huo kutokamilika licha ya kuwa uko nje ya muda wake wa kukamilika kwa miaka miwili sasa huku wananchi wakiendelea kuteseka.

mwisho.

Tuesday 24 November 2015

DED SUMBAWANGA APIGA MKWARA

Na Gurian  Adolf

Mkurugenzi wa Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa Hamidu Njovu amewaonya baadhi ya wakazi wa manispaa hiyo kuacha tabia ya kupuuza sheria ndogo zinazotungwa na halmashauri hiyo kwani ipo siku tabia hiyo itawatokea puani.

Akizungumza na gazeti hili mkurugenzi huyo alisema kuwa wapo baadhi ya watu kwa makusudi wakijua kuwa kunabaadhi ya vitu vinakatazwa na sheria ndogo za manispaa hiyo lakini wanakiuka makusudi bila hofu ya kuchukuliwa hatua.

Akitolea mfano amesema kuwa moja ya sheria hizo ni suala la usafi kwa kila mkazi wa manispaa hiyo lakini wapo baadhi ya watu wamekuwa na tabia ya kutapisha vyoo,kufanya biashara katika mazingira machafu bila kuwa na hofu ya sheria pamoja usalama wa afya zao.

Mkurugenzi huyo wa Manispaa amesema kuwa tayari ametoa maagizo kwa watendaji wa halmashauri hiyo kusimamia suala la usafi ili kuepukana na mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu kwani jitihada zisipofanyika ugonjwa huo unaweza kulipuka katika manispaa hiyo.

Aidha Njovu aliwataka vijana katika msimu huu wa kilimo kujishughulisha ili nyakati za mavuno weweze kupata mazao mengi ambayo yatawasaidia kupiga hatua katika maisha yao na familia zao.

Alisema vijana wanapaswa kutambua kuwa kunasheria ya nguvu kazi ambayo sasa imefika wakati lazima isimamiwe ipasavyo kwani wapo vijana wanaoshinda kijiweni bila kuzalisha huku wakiona mvua zinaendelea kunyesha na wao wamekuwa wakwanza kulia ugumu wa maisha.

Ameongeza kuwa huu ni wakati wa kutekeleza kaulimbiu ya Rais John Magufuli ya 'Hapa kazi tu" hivyo vijana hawanabudi kubadirika na kufanya kazi kwa bidii tofauti na hivyo watabaki wakililia ugumu wa maisha siku zote.

mwisho.

INYONGA KUMUONA RAIS MAGUFULI

 Gurian   Adolf

WAKAZI wa kijiji cha Inyonga wilaya ya mlele mkoani Katavi wamedai kuwa wanafunga safari na kwenda Ikulu kwa lengo la kumuona Rais  John Magufuli ili kumueleza kuchoshwa na umasikini ambao serikali imewasasabisha kutokana na kushindwa kuwalipa fedha za fidia.

Walimueleza hayo mkuu wa wilaya hiyo Said  Njiku wakidai kuwa wamesubiri kwa takribani miaka minne sasa bila mafanikio licha ya kwamba walihakikishiwa wangelipwa fedha hiyo ndani ya muda mfupi.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake Fransi Jerememia alisema kuwa wakati wilaya hiyo inaanzishwa wakazi hao waliombwa watoe eneo la ardhi ambalo walikuwa wakiishi,kulima na kufuga ili serikali ijenge hospitali ya wilaya kwa makubaliano ya kulipwa fidia lakini suala hilo limekuwa ni adhabu kwao.

Alisema kuwa baada ya kukubali ombi hilo la serikali waliambiwa waache kufanya ujenzi,kilimo,ufugaji na shughuli nyingine kwani watapewa fidia ili wakatafute maeneo mengine lakini hali imekuwa ni tofauti mpaka sasa wanaishi maisha ya dhiki kutokana na kutokuwa na ardhi.

‘’tulitegemea tungelipwa fidia ndipo tungeenda kununua ardhi ili tujenge na kuendelea na maisha yetu huko lakini mpaka sasa hakuna kinachoeleweka kwa hivyo tumechoka sasa ni kwenda kumuona rais tu ndiyo tunaamini atatusaidia serikali ya wilaya imeshindwa kabisa’’….alisema.

Naye Maria Simwanza mkazi wa kijiji hicho alisema kuwa mpaka sasa wamekwisha changishana fedha kiasi cha shilingi 800,000  fedha ambazo zitatumika kama naauri na kujikimu watu ambao watakwenda kumuona raisi kwani wanaishi maisha ya dhiki huku wakisikitika kuwa serikali ndiyo inayowatesa kwa kiwango hicho.

Alisema pamoja na kuwa mkuu wao wa wilaya ameahidi atalishughulikia suala hilo wamedai kuwa kila mara amekuwa akiwapa majibu ya kisiasa ambayo pia wameyachoka iliyobaki ni kumuona raisi tu huenda yeye atapatia ufumbuzi suala hilo kwani wanazidi kuwa masikini wa kutupa kutokana na kutokuwa na ardhi.

Hata hivyo mkuu huyo wa wilaya ya Mlele Said Njiku aliwasihi wananchi hao kuwa wavumilivu pamoja na changamoto hizo lakini wanapaswa kutambua kuwa serikali itawalipa na tatizo hilo litakwisha kabisa.

mwisho