Monday 19 March 2018

Mbunge atoa vitendea kazi

Na Gurian Adolf
Sumbawanga

MBUNGE wa viti maalumu mkoani Rukwa(CCM) Silafu Maufi ametoa msaada wa vitendea kazi vya ofisi kwaajili ya jumuia ya Umoja wa wanawake mkoani Rukwa(UWT) ili viweze kuwasaidia katika kurahisisha kazi zinazo wakabili watendaji wa jumuia hiyo.

Akikabidhi vitendea kazi hivyo jana ambavyo  ni ngamizi (Computer) aina ya DELL pamoja na  kichapishi (printer) mbunge huyo alisema kuwa kabla ya kustaafu kazi na kuchaguliwa kuwa mbunge wa viti maalum alikuwa akifanya kazi ya Katibu wa CCM katika wilaya mbalimbali hapa nchini.
Alisema kuwa katika utendaji wake wa kazi alikuwa akikabiliwa na changamoto kubwa ya ukosefu wa vifaa kitendo kilichosababisha kutekeleza majukumu yake kwa shida na wakati mwingine kutokwenda sambamba na muda. 

Maufi aliwaeambia wanachama wa UWT kutoka wilaya za Kalambo, Nkasi, Sumbawanga mjini na Vijijini kuwa kumekuwa na tatizo la uvujaji wa siri za ofisi na za chama pia hasa katika kipindi cha chaguzi mbalimbali na sababu moja wapo ni kutumia ngamizi za nje ya ofisi kuchapa kazi za chama na jumuiya yenyewe.

Kutokana na changamoto hiyo ametumia kiasi cha shilingi milioni 10 kununua ngamizi nne pamoja na vichapishi aina ya HP vinne kila kimoja na ngamizi yake kwa ajili ya ofisi za UWT katika ofisi za wilaya zote katika mkoa wa Rukwa.


Kwaupande wake Beata Weller ambaye  ni katibu wa UWT wilaya ya Kalambo alitoa shukrani kwa niaba ya makatibu wengine ambapo alisema kuwa walikuwa wanalazimika kusafiri kilometa 50 kutoka Matai Kalambo kwenda mjini Sumbawanga kwaajili ya kuchapa kazi za jumuiya na kutumia gharama kubwa na wakati mwingine walilazimika kulala huko kutokana na kuwa ofisi yao ilikuwa haina vifaa hivyo muhimu vya kutendea kazi.

Alisema kuwa  licha ya kutoa shukrani za dhati kwa mbunge Maufi pia wanatoa pongezi kwa mbunge huyo kukumbuka alikotoka na kujaribu kutatua changamoto za kiofisi maana wabunge wengi wanawafikiria wananchi peke yao na kusahau chama na jumuia zake.

Chama cha Mapinduzi mkoani Rukwa kinakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa vifaa vya ofisi, ukosefu wa ofisi ambapo wilaya za Sumbawanga vijijini na Kalambo hazina ofisi kabisa.

Mwisho

No comments:

Post a Comment