Tuesday 12 April 2016

Dc Sumbawanga aagiza baa kufunguliwa jioni

Na Gurian  Adolf
Sumbawanga

MKUU wa wilaya ya Sumbawanga mkoani Rukwa Methew Sedoyeka amepiga
marufuku biashara ya  kuuza pombe na vilevi vingine nyakati za asubuhi
badala yake biashara hiyo ianze kufanyika kuanzia saa 9;00 za mchana
baada ya muda wa kazi.

Akizungumza na vyombo vya habari ofisini kwakwe Methew Sedoyeka
alisema kuwa biashara hiyo imekuwa ikisababisha watu kunywa pombe
asubuhi na kushindwa kufanya kazi hali inayowasababisha washindwe
kujipatia kipato.

Alisema haiwezekani wilaya hiyo ikawa na walevi wengi kupita
wazalishaji kwa kufanya kazi na hivyo ameviagiza vyombo vya ulinzi na
usalama vya wilaya kuhakikisha vinachukua hatua kwa watu watakao kaidi
amri hiyo ya DC.

Aidha alitoa wito kwa wananchi wa Manispaa ya Sumbawanga pamoja na
wilaya ya Sumbawanga kujituma katika kazi ili waweze kupata kipato
kikubwa kitakacho wawezesha kujipatia maendeleo kutokana na nguvu kazi
yao.

Baadhi ya wakazi wa mji wa Sumbawanga wamepokea kwa mtazamo tofauti
agizo hilo la mkuu wa mkoa ambapo baadhi yao wamepongeza agizo hilo
huku wengine wakilalamikia kwamadai kuwa wao uzalishaji wao unatokana
na kuuza  vilevi na wanalipa kodi.

Mmiliki mmoja wa baa mjini humu Peter  Kayanda alisema kuwa wapo watu
kazi zao wanafanya nyakati za usiku kama walinzi na waliopo zamu za
usiku kazini muda wao wa kupumzika na kupata starehe unakuwa ni
asubuhi jioni ni muda wa kuelekea kazini.

Alisema kuwa pia serikali inapaswa kufahamu kuwa makampuni yanayouza
vilevi hapa nchini ndiyo yanaongoza kwa kulipa kodi tofauti na
makampuni ya uchimbaji wa madini hatua hiyo inaweza kusababisha
kupungua kwa mapato hata ya serikali.

Naye Monica Mayage mkazi wa Sumbawanga alisema kuwa kitendo hicho
kitasababisha pia watumishi walevi wa sekta binafsi na serikali kuwepo
kazini muda wote wa kazi na kuwajibika kwani baadhi yao wamekuwa
wakitoroka hata kazini kwajili ya kwenda kunywa pombe.

Mwisho

Wafugaji Mlele wamuangua DC

Na Gurian  Adolf
Mlele
WAFUGAJI wilayani Mlele mkoani Katavi wamemuangukia mkuu wa wilaya hiyo Issa Njiku wakimuomba asitishe kwanza  agizo lake la kuwataka waondoke katika mapori wanapofugia kwa madai kuwa maeneo hayo ni mapori tengefu.

Akiongea na  waandishi wa  habari  jana  mwenyekiti wa Chama  cha  wafugaji mkoa  wa  Katavi  (CCWT) Mussa  Kabushi  alisema   chama  cha wafugaji kinamwomba  mkuu huyo wa  Wilaya  asitishe  zoezi  alilopanga lianze kufanyika   Aprili  20  katika  Kata ya  Ugala  la kuwahamisha  wafugaji waliofuga mifugo  katika  mistu ya   Kata ya Ugala  katika  vijiji vya  Katambike  Kamili  na Kitongoji   Sanda.

Alisema kutokana na agizo la mkuu huyo wa wilaya la kuwataka wafugaji waondoke katika maeneo waliyopo hivi sasa linawasababishia usumbufu mkubwa na kuwafanya wajihisi kana kwamba wananyanyasika ndani ya nchi yao na wamekuwa wakifukuzwa fukuzwa hovyo bila utaratibu kama ni wakimbizi walioko ugegenini.

Kabushi alisema kuwa katika wilaya hiyo kuna mgawanyo wa matumizi ya ardhi ambapo
eneo walilotengewa wafugaji  ni  Ekta 3,765 sawa  na  hekta 9,430 ambalo linatosha  kulishia  mifugo   1,886 wakati  mifugo  iliyopo ni  zaidi ya  elfu  kumi .

Alisema kutokana na kutokuwa na eneo la kutosha kumesababisha wafugaji kuchungia mifugo hadi nje ya eneo walilotengewa hatua ambayo inatafsiriwa na serikali ya wilaya kuwa wamevamia katika maeneo ya hifadhi na hivyo kufukuzwa bila hata majadiliano.

Mwenyekiti huyo wa wafugaji alisema kuwa kwakuwa wakati mchakato wa ugawaji maeneo hayo unafanyika wafugaji hawakushirikishwa ni vizuri buasra za mkuu wa wilaya zikatumika na akaitisha mkutano ili zoezi hilo lifanyike upya kwa kuwashirikisha wafugaji ili kuondoa hata hatari ya mivutano baina ya wafugaji na wakulima.

Hivi karibuni Kwenye  mkutano  wa hadhara katika kata ya Ugalla wilayani humu,mkuu  huyo wa  Wilaya aliagiza ifikapo April 20 wafugaji wote wanaochungia ng'ombe katika hifadhi na maeneo mengine ambayo ni tengefu  waondoke mara moja  pia  aliwataka  wafugaji hao wapunguze mifugo yao ambapo aliwasahauri  waipunguze hadi kufikia mwenye ng'ombe 200 abaki na 100 na mwenye 100 abaki na 50.

Mwisho

Serikali ya kijiji yawaonya wafugaji kutembea na silaha za jadi



Na Gurian Adolf
Nkasi.

SERIKALI ya kijiji cha Ntatumbila wilayani Nkasi Mkoani Rukwa imewapiga marufuku watu wa jamii ya wafugaji kwenda maeneo ya starehe wakiwa na silaha za jadi ikiwemo mapanga hali ambayo inahatarisha usalama wa eneo husika.

Mwenyekiti wa kijiji hicho Ignas Kanjele alipiga marufuku hiyo katika mkutano wa kijiji uliofanyika jana uliokuwa na lengo la kuzungumzia hali ya usalama pamoja na kutoa taarifa ya mapato na matumizi ya kijiji hicho.

Alisema kuwa katika kijiji hicho kumekuwa na tabia ya muda mrefu kwa wafugaji kutembea wakimwa na sime, mkuki, mapanga na hata marungu hali inayosababisha hofu kwa baadhi ya wananchi kwani hawajui usalama wao wanapokutana na mtu huyo.

Mwenyekiti huyo wa ulinzi na usalama wa kijiji hicho alisema kuwa kutokana na kutembea na silaha hizo bila serikali yake kuchukua hatua baadhi yao wamekuwa wakiwapiga wananchi na hata kuwajeruhi hali ambayo haivumiliki kijijini hapo.

“ kuanzia leo hii ni marufuku kwa wafugaji kutembea na silaha za jadi kwakua hii inasababisha wawapige wananchi fimbo na kuwaumiza huku wengine wakienda katika sehemu za starehe kama harusini, mpirani wakiwa na fimbo na sime atakaye kamata atachukuliwa hatua”

Aidha aliliagiza jeshi la mgambo kijijini hapo kuhakikisha kuwa wanawasaka watakaokiuka amri hiyo ili kuondoa vitendo vya uvungaji sheria kwani hata migogoro ya wakulima na wafugaji inatokana na wengine kutembea na silaha hali inayosababisha kundi jingine litumie silaha yanapokabiriana makundi haya mawili.

Kufuatia marufuki hiyo baadhi ya wakazi wa kijiji hicho wakizungumza na gazeti hili waliushukuru uongozi wa kijiji hicho walidai kuwa tabia hiyo imekuwa ikiwakera kwa muda mrefu lakini walikuwa hawana namna ya kufanya.

Monica Kavishe mkazi wa kijiji hicho alisema kuwa baadhi ya wafugaji hao wamekuwa wakiwachapa fimbo na kuwajeruhi na wamekuwa wakifanya ubabe kijijini hapo kwa madai kuwa wanauwezo hata wa kifedha wa kuwadhibiti viongozi wa serikali lakini kutokana na maamuzi ya mwenyekiti Kanjele inaonesha ameamua kwenda na kasi ya serikali ya awamu ya tano ya rais John Magufuli.

Mwisho