Monday 4 November 2013

POLISI WAPEWA SOMO KUHUSU UKATILI WA KIJINSIA DHIDI YA WATOTO



Naibu Kamishina wa Polisi, Bi Adolfina Chialo akifunga mafunzo ya siku tano kwa maofisa wa polisi kuhusu unyanyasaji, na ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto jana. kwa habari zaidi soma hiyo hapo chini.

Na Gurian Adolf, Sumbawanga.

MEELEZWA kuwa Jeshi la polisi nchini linaweza kuwa chachu ya kukomesha kabisa vitendo vya ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto iwapo askari polisi wanashughulikia matukio hayo watatunza taarifa za siri wanazofikishiwa na watoa taarifa.

Naibu kamishna wa polisi, Adolfina Chialo alisema hayo wakati akifunga mafunzo ya siku tano yaliyowashirikisha askari polisi kutoka mikoa ya Rukwa na Katavi wanashughulika kutoa huduma katika dawati la kupinga unyanyasaji wa kijinsia na ukatili kwa watoto katika mikoa hiyo.

''Kutoa huduma bora kwa mteja ni lazima na kila afisa wa polisi anapaswa kujua hivyo kwani ndio kiini cha kuendelea kupata taarifa na usiri unahitaji sana, maana baadhi ya Polisi hawana usiri pindi wapopatiwa taarifa sasa mkibadilika mnaweza kuwa chachu ya kukomesha unyanyasaji na ukatili dhidi ya watoto” alisema Kamishina huyo wa polisi.

Aliongeza kuwa polisi wanapaswa kutambua kuwa kutoa huduma bora kwa wateja ni suala la lazima na wala sio hiari yao kwani wao wanashughulika na jamii hivyo basi kuhakikisha wanaitengenezea mazingira mazuri jamii hiyo ni wajibu wao tofauti na hivyo watakuwa wanachukiwa na wananchi.

Naibu Kamishina huyo alisema kuwa daima watoto wadogo wanapotendewa vitendo hivyo na iwapo wasipohudumiwa vizuri wanabaki na hali hiyo vichwani mwao na wanapokuwa watu wazima nao hutenda vitendo kama hivyo kwa watoto wadogo kitu ambacho ni hatari kwani uzembe wa watendaji unaweza kusababisha kuandaa wanyanyasaji wa miaka ijayo.

Awali akimkaribisha Kamishna huyo kufunga mafunzo hayo kamanda wa polisi mkoa wa Rukwa, Jacob Mwaruanda ,alisema kuwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia pamoja na ukatili kwa watoto vipo sana mkoani humo jeshi la polisi wanajitahidi kuvishughulikia kwa mujibu wa sheria.

Alisema kuwa jamii ya wakazi wa mkoa huo wanatakiwa kushiriki katika kutokomeza vitendohivyo lakini ikiwaachia polisi peke yao itakuwa ni jambo gumu sana kwani watambue kua wanao athirika ni watoto wao hivyo mapambano haya ni lazima washiriki na si kuwaachia polisi tu 
Baadhi ya Maofisa wa polisi wakiwa katika picha ya pomoja na viongozi wao mara baada ya kumaliza mafunzo ya siku tano kuhusu unyanyasaji na ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto yaliyofanyika katika ukumbi wa Hotel ya Holland mjini Sumbawanga.