Sunday 23 April 2017

Watoto waliougua ugonjwa wa ngozi Afya zao zaendelea kuimarika.

Israel Mwaisaka
Nkasi

WATOTO waliougua ugonjwa wa ngozi na kutengwa katika kijiji cha Nkata kata ya Kate  wilayani Nkasi afya zao zimeendelea kuimarika kutokana na matibabu wanayoyapata kutoka kwa mganga wa magonjwa ya ngozi katika kituo cha afya cha Nkomolo wilayani Nkasi.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya Nkasi Julius Mseleche Kaondo alionyesha kufurahishwa na maendeleo ya watoto hao baada ya kuwatembelea jana na kuweza kujionea maendeleo ya kiafya ya watoto hao toka waanze kutibiwa katika hospitali hiyo.

Akizungumza katika kituo hicho cha afya Mkurugenzi huyo alimtaka Daktari huyo kufanya awezalo ili kuweza kuwarejesha wagonjwa hao katika hali yao ya kawaida hasa kutokana na jinsi watoto hao walivyoathirika na ugonjwa huo wa ngozi.

Alisema kuwa halmashauri itagharamia gharama zote za matibabu na chakula katika kipindi chote cha matibabu kwa watoto hivyo kutaka umakini mkubwa wakati wa kutoa huduma kwa watoto hao.

Mganga wa magonjwa ya ngozi anayewahudumia watoto hao Hillary Daukajambonye alimweleza mkurugenzi mtendaji huyo kuwa ameugundua ugonjwa unawatesa watoto hao ambao umedumu kwa muda wa miaka sita bila ya matibabu na kuwa huenda wakapona ndani ya wiki moja hasa ni kutokana na kuwepo kwa dawa za kuwatibu watoto hao.

Alisema ugonjwa huo unatibika na kilichobaki sasa kwa watoto hao ni suala zima la lishe na inaonekana mazingira wanayoishi lishe ni duni na kuwa vile halmashauri itatoa fedha itawasaidia watoto hao kupata lishe na mavazi ili watoto hao waweze kuwa na nguo za kubadilisha kila wakati ili kuweza kukabiliana na wadudu wanaosababisha ugonjwa huo .

Baba mzazi wa watoto hao Martin Kazumba aliishukuru serikali kutokana na uamuzi wao wa kuichukua familia yake na kuanza kuitibu kwani ugonjwa huo umeitesa familia yake kwa kipindi cha miaka sita na kutokana na uduni wa maisha alishindwa kutafuta tiba ya ugonjwa huo katika familia yake

Watoto hao ambao ni Petro na Lucas Kazumba walipozungumza na mwandishi wa habari hizi walidai kuwa walikua wamekata tamaa ya kuishi lakini sasa wameanza kuiona faraja baada ya kuanza matibabu.

Mkuu wa mkoa alimuagiza mganga wa hospitali ya mkoa wa Rukwa kuhakikisha kuwa watoto hao wagonjwa wa ngozi ambao wametengwa na jamii kutokana na ugonjwa huo kwa kipindi kirefu sasa kuhakikisha kuwa wanapata matibabu na halmashauri ya wilaya Nkasi kuchukua hatua mara moja.

Ugonjwa wa watoto hao uliripotiwa kwenye vyombo vya habari ambapo mkuu wa mkoa Rukwa Zellote Steven kuchukua hatua mara moja baada ya kupata habari hizo.
mwisho

No comments:

Post a Comment