Na Gurian Adolf
Sumbawanga
WAZIRI wa afya,maendeleo ya jamii,jinsia na watoto Ummy
Mwalimu ametoa siku saba kwa wanawae wote waliochukua mikopo katika benki ya
wanawake wawe wamerudisha vinginevyo waanze kuchukuliwa hatua za kisheria.
Alitoa agizo hilo jana wakati alipokuwa mgeni rasmi
akihutubia katika sherehe za wanawake zilizofanyika katika uwanja wa Nelson Mandela
mjini Sumbawanga.
Alisema kuwa benki ya wanawake imekuwa ikitoa mikopo lakini
kitu cha kusikitisha baadhi yao wamekuwa na tabia ya kurudisha mikopo hiyo
kitendo kinachowanyima fursa wanawake wengine ya kunufaika na mikopo hiyo.
Waziri Ummy alisema kuwa anatoa siku saba wanawake wote
wanaodaiwa mikopo na walipaswa kuwa wamesharudisha wahakikishe wamerudisha
katika kipindi cha siku saba tofauti na hivyo watachukuliwa hatua kali za
kisheria.
Pia waziri huyo alitumia fursa hiyo kumuomba waziri wa
utawala bora George Mkuchika kuwafikisha mahakamani wanawake wote waliokuwa
watumishi wa benki hiyo ambao walifanya ufisadi kwani wamekuwa ni kikwazo kwa
maendeleo ya wanawake wenzao.
Alisema kuwa benki hiyo iliajiri wanawake ikiamini kuwa
watakuwa na uchungu na benki yao ambapo wataisimamia vizuri ili iweze kuendelea
zaidi na kuwa msaada lakini kinyume na matarajio wanawake hao ndio wamefanya
ufisadi na kuendelea kuwakwamisha wanawake wenzao.
‘’nitumie fursa hii kumuomba kaka yangu waziri wa utawala
bora Geore Mkuchika kuwafikisha mahakamani wanawake wote ambao walikuwa
watumishi wa benki ya wanawake na kisha kufanya ufisadi kwani hawa ni adui wa
wanawake wenzao’’ alisema.
Waziri huyo alitumia fursa hiyo kuwaagiza wakurugenzi wa
halmashauri zote nchini kufikiria upya katika suala la kutoa mikopo kwa makundi
ya wanawake na vijana kwani mikopo inayotolewa haiendani na uhalisia kwakuwa
haiwezekani kikundi cha watu 15 wakakopeshwa shilingi 300,000 halafu ukategemea
watapiga hatua.
‘’Naagiza wakurugenzi wote nchini kutazama upya suala la
mikopo ya wanawake na vijana inayotoka katika asilimia tano ya mapato ya
halmashauri kuwakopesha mikopo itakayowasaidia kufanya shughuli na kupata faida
kwasababu utakuta kikundi cha watu 15 wanapewa shilingi 300,000 fedha ambazo
hazitoshi walau ziwe hata shilingi milioni kumi kwa kikundi walau wanaweza
kuzizalisha’’ alisema.
Pia aliitaka jamii kubadili mtazamo wa kufikiria kuwapelekea
misaada ya chakula na nguo watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu badala yake waanze kuwalipia
huduma ya afya kupitia Toto Afya Kadi kwani miongoni mwa changamoto zinazo
wakabiri watoto hao ni pamoja na huduma za afya.
Naye mbunge wa jimbo la Sumbawanga mjini Aesh Hilary
alimuomba waziri huyo magari ya kubebea wagonjwa ambapo wanawake hasa
wajawazito ambao wanahitaji huduma za dharula kwakua mkoa huo wa Rukwa
unachangamoto ya upungufu wa magari hayo.
Baada ya kulisikia ombi hilo waziri huyo wa afya aliahidi
kutoa magari mawili ya kubebea wagonjwa(ambulance) ambapo moja litakuwa
kwaajili ya hospitali ya rufaa ya Sumbawanga na jingine aliagiza kuwa kitafutwe
kituo kilichopo mbali na mjini ndiyo kipatiwe gari hilo.
Naye mkuu wa Kalambo Julieth Binyura alimshukuru waziri Ummy
kwa kukubali kufika mkoani Rukwa na kusherekea na wanawake wa mkoa huo kwani
amewapa hamasa na kuwasaidia kutatua changamoto nyingi ambazo zitawafanya
kuongeza ari katika utendaji kazi.
Mwisho
No comments:
Post a Comment