Thursday 20 July 2017

Wakazi wa Kata ya Malangali wafurahia ujenzi wa kiwanda

Na Gurian Adolf
Sumbawanga
WAKAZI wa kata ya Malangali Sumbawawanga mjini wamefurahishwa na hatua ya mwekezaji wa kiwanda cha kusaga unga wa mahindi katika kata hiyo ambapo kitatoa ajira kwa vijana wa kata hiyo wasiokuwa  na ajira.
Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi wakazi hao walisema kuwa mwekezaji huyo anayeitwa Asayile Paulo Msaku almaarufu kwa jina  la  london  ni mwekezaji mkazi wa eneo hilo ambaye anapaswa  aungwe mkono.
Mmoja wa vijana wa kata hiyo Peter Kasanzya alisema kuwa kutokana na ujenzi wa kiwanda hicho mwekezaji huyo ameonesha dhamira ya kuiunga mkono serikali ya awamu ya tano  ambayo inasisitiza ujenzi wa viwanda.
Alisema kuwa kutokana na ujenzi wa kiwanda hicho vijana watapata  ajira ambapo wataboresha maisha yao kwani watakua wamepata sehemu ya kufanyia kazi na hawatahangaika tena kutokana na kukosa ajira.
Naye mwekezaji huyo London alisema kuwa kiwanda hicho kimefuata taratibu zote za usalama wa Mazingira na tayari wataalamu wa Mazingira wamethibitisha kuwa hakuna athali zozote za Ki Mazingira zinazoweza kutokea. 
Alisema kuwa kiwanda hicho kikikamilika kitatoa ajira zaidi ya 100 kwa vijana wa kata hiyo ambapo watanufaika kwa kujipatia kipato na kuwa na uhakika wa maisha kutokana na ujira watakaopata kwa kufanya kazi.
Aliwasihi wananchi wa kata hiyo wamuunge mkono kwani kiwanda hicho kitakuwa ni cha mfano na hakitasababisha usumbufu wowote kwa kutoa  moshi pamoja na kelele kwani vyote hivyo vimezingatiwa ili kuto wabugudhi wananchi wa kata hiyo.
Mwisho

No comments:

Post a Comment