Tuesday, 22 August 2017

Walimu wanne wafundisha wanafunzi 380


Na Gurian Adolf
Katavi
WALIMU wanne wa shule ya msingi Makongolo iliyopo katika Kata ya Magamba Manispaa ya Mpanda wanalazimkia kufundisha wanafunzi 380 kuanzia darasa la awali hadi la nne na wote wanafundishwa Katika vyumba viwili vya madarasa.
Mbali ya matatizo hayo shule hiyo pia ina matundu mawili  ya vyoo kwa ajili ya wanafunzi huku walimu wakiwa hawana choo cha shule hivyo wanalazimika kutumia choo kilipocho katika nyumba ya mwalimu mkuu wa shule hiyo .
Akizungumza kwa sharti la kutoandika jina lake gazeti mmoja wa walimu wa shule hiyo ambayo iko umbali wa kilomita kumi  kutoka mjini Mpanda alisema kuwa shule hiyo pia haina ofisi ya walimu ambapo wanalazimika kufanya shughuli zao chini ya miti.
“Najisikia vibaya sana  kwenda  kujisaidia kwenye choo  kilichopo  kwenye nyumba ya mwalimu mwenzetu kwa kuwa shule haina choo kwa ajili ya walimu…pia kutokana na uhaba wa vyumba vya madarasa ambavyo vipo viwili tu wanafunzi  wanafundishwa kwa zamu"alisema mwalimu huyo.
Alisema kutokana na  uhaba wa  madarasa na uchache wa  walimu  wanalazimika wanafunzi wa shule hiyo kufundishwa kwa  zamu  huku wengine wakisomea chini ya miti.
Mwenyekiti wa kijiji hicho Hosea Mpagasi akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea shule hiyo jana alisema kuwa shule hiyo ilianzishwa  na  kusajiliwa rasmi mwaka 2014.
“Shule hii  inakabiliwa na uhaba mkubwa wa walimu ambapo wapo walimu  wanne tu hivyo mmoja wao akiugua au kupata dharura  ina kuwa mzigo mkubwa kwa waliobakia “ alieleza.
Kwa  upande wake Diwani wa  Kata ya Magamba Filipo Kalyalya alisema kuwa yeye kama mwakilishi wa wananchi katika kata hiyo hafurahishwi hata kidogo na changamoto hizo zinazoikabili shule hiyo huku akidai kuwa uongozi wa kata umekuwa ukichukua hatua mbalimbali  ili kuinusuru shule hiyo lakini umekuwa ukikwamishwa na viongozi wa  kijiji hicho .  
Alisema kuwa Kampuni ya Ujenzi ya Kichina  inayokarabati barabara  inayounganisha Mji wa Mpanda na Kijiji cha Sitalike kwa kiwango cha lami  ilitoa msaada wa matofali 400 kwa ajili ya ujenzi  wa vyumba vya madarasa  lakini ni matofauli 40 tu yaliyofikishwa shuleni hapo huku mengine hayaeleweki yalipopelekwa na uongozi wa kijiji hicho.  
“Nilipofuatilia Kampuni ya Ujenzi ya Kichina ilinithibitishia kuwa matofali yote 400 iliyotoa kama msaada kwa  shule hiyo yalikabidhiwa uongozi wa kijiji cha Makongolo “ alisema diwani huyo .
Alisema kuwa atahakikisha kabla ya msimu wa mvua za masika kuanza Novemba mwaka huu ujenzi wa matundu ya vyoo vya wanafunzi  wa shule hiyo vinaanza kujengwa  ili kuwaepusha kukumbwa na magonjwa ya kuharisha  ikiwemo kipindupindu.
Mwisho

No comments:

Post a Comment